Marekani yataka vita Ukraine vikomeshwe ifikapo Juni

Chanzo cha picha, Getty Images
Rais wa Ukraine Volodymir Zelensky, amesema kwamba Marekani imeitaka nchi yake na nchi jirani ya Urusi kumaliza vita yao inayoendelea ifikiapo mwezi Juni mwaka huu.
Kiongozi huyo ameongezea kwamba, pande hizo mbili zinazozozana zimepokea mualiko kuhudhudria kikao cha mazungumzo nchini Marekani wiki ijayo.
‘Marekani imependekeza kuwa kwa mara ya kwanza makundi yanayowakilisha mataifa hayo mawili - yafanye kikao cha ana kwa ana nchini Maekani wiki inayokuja, na kuongezea kwamba vikao hivyo vifanyike katiak mji wa Miami. Ukraine imethibitisha kushiriki kwenye mkutano huo,’ alisema.
Washington na Moscow hawajalizungumzia suala hilo, ila Rais wa Marekani Donald Trump amekuwa akipendekeza wazo la kutaka vita hivyo kukoma na mzozo kumalizwa tangu aliporejea madarakani mwaka mmoja uliopita. Wakati huo huo, Urusi imeendeleza mashambulizi yake yanayolenga miundo mbinu mbalimbali ya nishati, hali inayosababisha maeneo mengi zaidi kukosa umeme.
Katika taarifa aliyowasilisha mapema leo, Zelensky aliwaambia wanahabari kuhusu yaliyojiri katika vikao vilivyoandaliwa Abu Dhabi, ambavyo vilikamilika Ijumaa wiki hii, ambapo hakukuwa na ripoti yoyote kuhusu hatua iliyopigwa ya kutatua mzozo. Zelensky amesema; ‘Masuala magumu yamesalia yalivyo, magumu,’ ikiwemo suala la Urusi kukalia maeneo yaliyo chini ya himaya ya Ukraine, huku Ukraine ikitakiwa kuachilia maeneo hayo kumilikiwa kikamilifu an Urusi.
Amesema kwamba, pande husika zilijadili, kwa mara ya kwanza, uwezekano wa kufanyika mkutano utakaowahusisha viongozi wa nchi hizo tatu, na wala sio wajumbe wa nchi hizo, ila ameonya kuwa ‘maandalizi maalumu‘ ni sharti yafanyike kwa hilo kufanikiwa.
Alipoulizwa ikiwa kuna muda uliowekwa kwa makubaliano kuafikiwa, kiongozi huyo wa Ukraine alijibu: ‘Wamarekani wanasema wanataka kukamilisha kila kitu ifiakiapo mwezi Juni. Ni kwanini hilo lifanyike kabla ya msimu wa joto kali kuanza?’ aliendelea kusema. ‘Tunaelewa kuwa masuala yao ya ndani yatakuwa na uzito na athari kubwa kwenye mzozo huu kati yetu.’









